Friday, June 19, 2015

DK Shein: Nitawashinda wapinzani Zanzibar Oktoba

0

Zanzibar. Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Dk Ali Mohamed Shein jana alichukua fomu ya kuomba ridhaa ya chama chake kuteua tena kugombea urais wa Zanzibar huku akitamba kuwa ataendeleza wimbi la ushindi dhidi ya wapinzani katika Uchaguzi Mkuu ujao.
Alisema iwapo chama chake kitampitisha na kupewa ridhaa na wananchi, atahakikisha Serikali yake inafanya kazi kwa kuzingatia misingi ya utawala bora na uwazi.
Akisindikizwa na makada wa CCM, Dk Shein alisema katika kipindi chake cha uongozi cha miaka mitano inayomalizika, Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) imefanikiwa katika utekelezaji wa ilani ya uchaguzi na kuimarisha misingi ya umoja wa kitaifa.
Baada ya kukabidhiwa fomu hiyo na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai katika Makao Makuu ya CCM Kisiwandui Mkoa wa Mjini Magharibi, Dk Shein aliwaambia viongozi wa mikoa sita ya kichama kuwa wakati anaingia madarakani mwaka 2010, aliweka misingi imara ya utawala bora kwa kufanya tathmini ya utendaji kwa kukutana na kila wizara baada ya miezi mitatu kuangalia matatizo na mafanikio.
“Kama kawaida yangu napenda kuwahakikishia kuwa nitaongoza Serikali yenye uwazi, uwajibikaji na yenye uwezo wa kutimiza majukumu yake na kulinda misingi ya haki za binadamu, sheria na Katiba,” alisema Dk Shein.
Alisema lengo kubwa la serikali yake ni kujenga uchumi imara na kuendeleza malengo ya kuimarisha sekta ya kilimo, uvuvi, viwanda na sekta ya uwekezaji ili kuinua Pato la Taifa na wananchi wa Zanzibar.
Alisema ni jambo la faraja kuona uchumi wa Zanzibar umekuwa kwa asilimia saba kutoka asilimia 2.6 ya mwaka 2010, huku uwezo wa ukusanyaji mapato ukifikia Sh35 bilioni kutoka Sh13.5 bilioni kwa mwezi mwaka 2010.
Alisema iwapo CCM itampatia tena ridhaa na kuchaguliwa na wananchi kuendelea na wadhifa huo wa urais, atahakikisha anaendelea kulinda misingi ya Mapinduzi na Muungano.
“Kuna watu wachache wanautia chokochoko Muungano na Mapinduzi yetu, msiogope, tutawashughulikia kwa mujibu Katiba na sheria bila ya kutumia nguvu,” alisema na kuibua shangwe za CCM...CCM...
Alisema ili Zanzibar iweze kupiga hatua kubwa ya maendeleo baada ya uchaguzi mkuu, atahakikisha amani na utulivu vinapewa nafasi kubwa.
Alisema hatakuwa na mzaha katika kusimamia misingi ya utawala wa sheria na hakuna mtu ambaye ataonewa katika uongozi wake... “Mimi ni muumini wa Kiislamu, sitomdhulumu mtu, najua kwamba kumdhulumu mtu ni dhambi, nitatenda haki na yeyote atakayeleta chokochoko na Zanzibar sitamuachia kwa manufaa ya Zanzibar na wananchi wake.”
Ushindi wa CCM
Alisema suala la ushindi kwa CCM halina mjadala kutokana na kazi kubwa iliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Saba katika ujenzi wa miundombinu, ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Abeid Amani Karume, kuboresha masilahi ya watumishi wa umma na kudumisha amani na umoja wa kitaifa
Akisindikizwa na nyimbo za hamasa za CCM, Dk Shein, aliwarushia vijembe wapinzani na kuwa ataendeleza wimbi la ushindi katika uchaguzi wa mwaka huu, akiamini mtaji wake ni utekelezaji wa ilani... “Wembe ni uleule wa ushindi kwani hao wote nitakaoshindana nao nilishindana nao 2010 na nikawashinda.”
Aliwashangaa wanaozungumzia mafanikio ya mradi wa uwanja wa ndege wa Zanzibar na mpango wa ujenzi wa bandari huru wakati hiyo ni utekelezaji wa ilani ya CCM na mpango wake ulianza wakati wa utawala wa Rais mstaafu, Dk Salmin Amour.
Wagombea sita
Tayari wagombea sita wametangaza nia kuwania urais wa Zanzibar wote kutoka Pemba. Wagombea hao Dk Shein, Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, mlezi wa chama cha ADC, Hamad Rashid Mohamed, Katibu Mkuu wa Tadea, Juma Ali Khatib Mwenyekiti wa Chama cha Wakulima Tanzania (AFP), Saidi Soud na Makamu Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, Ambar Khamis Haji.
Author Image

About tzfleva
Soratemplates is a blogger resources site is a provider of high quality blogger template with premium looking layout and robust design

No comments:

Post a Comment