Wednesday, February 25, 2015

Warioba: Ipo siku maadili yataingizwa kwenye Katiba

0

Dar es Salaam. Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba amesema nchi haiwezi kupambana na mmomonyoko wa maadili ya viongozi wa umma kama haitakubali kuingiza suala la maadili katika Katiba.
Amesema sheria ya maadili ya viongozi wa umma haina nguvu ya kukabiliana na mmomonyoko huo na  inakosa meno kwa sababu inasimamiwa na watu walewale wasiotaka ‘kuguswa’.
“Kuna mambo yanakataliwa sasa hivi, lakini kuna siku lazima yatakuja kuingizwa katika Katiba, mfano ni suala la maadili,” alisema Jaji Warioba wakati akizungumza katika kipindi cha Dakika 45 kilichorushwa na ITV juzi usiku.
“Hatuwezi kuendelea kama ilivyo sasa bila kuchukua hatua kali na nzito kushughulikia maadili. Lazima kuna siku suala hili litaingia katika Katiba tu,” alisema.
Jaji Warioba ametoa kauli hiyo ikiwa zimepita siku mbili tangu Baraza la Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kutaja viongozi wa umma itakaowahoji kutokana na kuhusika katika kashfa ya Akaunti ya Tegeta Escrow.
Miongoni mwao yupo kigogo wa Ikulu mwenye cheo cha mnikulu, Shaban Gurumo, aliyekuwa Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka na aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo na mwanasheria mkuu wa zamani, Andrew Chenge.
Katika rasimu ya pili ya Katiba, Tume ya Jaji Warioba ilipendekeza miiko na kanuni za uongozi kama tunu za Taifa, lakini Bunge Maalumu la Katiba iliyaondoa na kuyaweka katika msingi wa utawala bora.
Mara kadhaa Jaji Warioba amekuwa akihoji kuwa uzalendo na uadilifu si mpaka mtu awe kiongozi, kwamba mambo hayo mawili si misingi ya utawala bora ni misingi ya kitaifa na inamhusu kila Mtanzania.
Akifafanua zaidi suala la maadili katika kipindi hicho, Jaji Warioba alisema tume yake iliangalia sheria ya maadili ikaona haina nguvu sana na inategemea kiongozi mmoja na ndiyo maana waliingiza suala hilo katika rasimu ya Katiba
“Tuna sheria ya maadili lakini haina nguvu kwa sababu wanaoisimamia ni walewale. Nchi za Ufilipino (Philippines), Afrika Kusini, Namibia na Kenya walikuwa na sheria lakini haikuwa na nguvu na iliwahusu watu walewale. Waliamua kuweka maadili katika Katiba ili waweze kulitekeleza vizuri,” alisema.
Alisema maadili pia yanawahusu viongozi lakini wakati huo huo viongozi hao ndiyo wanaosimamia sheria ya maadili, hivyo hawawezi kukubali liwemo jambo litakalowadhuru.
Jaji Warioba alieleza jinsi Azimio la Arusha lilivyokuwa na nguvu, akifafanua kuwa suala la maadili lilijipambanua wazi  na waliokuwa wakitenda mambo kinyume walijiondoa wenyewe bila kusubiri kuondolewa.
Akigusia suala la maadili na sakata la mabilioni ya fedha yaliyochotwa katika Akaunti ya Tegeta Escrow alisema, “Katika suala la escrow niliuliza nani msafi…, we subiri tu si tunakwenda katika uchaguzi mkuu viongozi watakuwa na fedha nyingi sana.”
Kura ya maoni isubiri 2016
Akizungumzia daftari wa wapigakura na upigaji wa Kura ya Maoni kupitisha Katiba Inayopendekezwa, alisema, “Nia ya kupitisha Katiba mpya mapema ilikuwa na lengo la kuitumia katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, lakini inahitaji maandalizi. Mfano Katiba Inayopendekezwa ina sehemu ya Tume ya Uchaguzi na kama ukiipitisha, utaunda upya tume hiyo na suala hilo linahitaji muda.”
Alisema ili kufanikisha uundwaji wa tume hiyo ni lazima Bunge likutane, lakini mpaka itakapofika siku ya kuipigia kura Katiba hiyo na kuipitisha, Bunge litakuwa limekwishakaa na hakutakuwa na uwezekano wa kubadili lolote.
“Hakuna haja ya kuharakisha, ni vizuri twende taratibu ili tusije tukafanya makosa ambayo yatatuletea matatizo,” alisema.
Aliongeza, “Itakuwa vizuri kama kura ya maoni ikasitishwa mpaka mwaka 2016. Inaonekana tutalazimika kusubiri na hii inatokana na matatizo tu ya kawaida ya kutokuwa na daftari la Wapigakura.
Mgongano wa maslahi
Jaji Warioba pia aligusia kitendo cha wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kuruhusiwa kugombea nafasi za kisiasa baada ya kumalizika kwa Bunge hilo, akisema kuwa hilo lilikuwa kosa kubwa.
“Uganda tume ilipomaliza kazi, wananchi walichagua Bunge la Katiba na sharti moja ni kwamba ukiingia katika Bunge hilo hauruhusiwi kugombea uongozi. Walijua kazi yao ni kupitisha Katiba tu,” alisema.
Alisema kosa lililofanyika nchini ni kuruhusu wabunge waliopitisha Katiba kugombea, hivyo kuwafanya baadhi kuondoa masuala ya msingi waliyoona kuwa ni kikwazo kwao katika uchaguzi.
“Nadhani hiyo ni kasoro tuliyokuwa nayo na tulipeleka watu ambao wana malengo na Katiba kwa manufaa yao binafsi,” alisema.
Kuhusu maridhiano kuelekea upigaji wa Kura ya Maoni alisema, “Suala la maridhiano lilipofika kwenye vyama vya siasa likabadilika na sasa tunazungumzia maridhiano ya vyama vya siasa. Maridhiano ya vyama vya siasa siyo lazima yawe maridhiano ya wananchi.”Jaji Warioba pia alizungumzia suala la muungano, kueleza historia ya mfumo wa uteuzi wa viongozi wa Serikali ya Muungano na Zanzibar ili kuondoa dhana ya upande mmoja kuonekana unatoa viongozi wengi kuliko mwingine.
Author Image

About tzfleva
Soratemplates is a blogger resources site is a provider of high quality blogger template with premium looking layout and robust design

No comments:

Post a Comment